HAKIKISHA UNAISHI MAISHA ULIYOKUSUDIWA UKIJUA KUSUDI LA UWEPO WAKO LIMEFUNGWA KWENYE MUDA

0
5KB

Mtu hakuumbwa (hakuzaliwa) kwa bahati mbaya bali kwa kusudi maalum la Mungu. Mungu ndiye ameridhia mtu huyo awepo duniani ili amtumie kufanikisha makusudi yake duniani. Kosa letu ni kufikiri maisha yetu yanafanana, pia muda na makusudi ya uwepo wetu vinafafana. Kila mmoja wetu ana muda wake na kusudi lake la kutekeleza awapo chini ya jua, ndio ana wajibu mahususi wa kuwepo kwake hapa duniani na hivyo sharti ajue kwa nini yupo na aishi kulitekeleza kusudi hilo.

Ndio, kosa letu ni kuishi kwa kuangalia wengine wanaishije, wanafanya nini na kutaka kuwa kama wao ilihali ndani ya kila mmoja kuna uwezo na neema ya pekee ya kumsaidia kuishi alivyokusudiwa na kisha kuwa kiungo cha wengine kufanikiwa. Hivyo ni wajibu wa kila mmoja wetu kumtafuta na kumjua Mungu ili amsaidie kuishi maisha aliyokusudiwa akijua kusudi la uwepo wake limefungwa kimuda. Hivyo ili kufanikiwa kuishi maisha uliyokusudiwa unahitaji kujua na kufanya yafuatayo:

Jambo la kwanza: Tafuta kujua kusudi la Mungu kwenye maisha yako na namna ya kulitekeleza.

Isaya 46:9-10 imeandikwa Kumbukeni mambo ya zamani za kale; maana mimi ni Mungu, wala hapana mwingine; mimi ni Mungu, wala HAPANA aliye kama mimi; nitangazaye MWISHO tangu mwanzo, na tangu zamani za kale MAMBO yasiyotendeka bado; nikisema, SHAURI langu litasimama, nami nitatenda mapenzi yangu yote’ (Mithali 16:4).

Mungu anayo mambo (makusudi) kwa kila mmoja wetu ambayo anataka yatimizwe duniani kupitia mtu husika. Ndio, kabla mtu hajazaliwa, Mungu alishapanga nini mtu huyo atafanya atakapomruhusu kuja duniani na hivyo ni jukumu la mtu kuyatafuta na kuyajua makusudi ya uwepo wake na kuishi katika hayo. Kila mmoja wetu ana kusudi kuu la uwepo wake sambamba na makusudi maalum/mahususi kwa muda maalum. Makusudi hayo ni ya Mungu ila anayetekeleza kupitia mtu, chini ya jua.

Mungu huwapa neema na kuwaweka wanadamu kwenye mazingira na nafasi mbalimbali kadri apendavyo ili watekeleze makusudi yake. Mungu anatarajia watumie mazingira na nafasi hizo kuhakikisha makusudi yake makuu na mahususi yanatimizwa vinginevyo wanamchukiza (1Samweli 15:1-11, Esta 4:14). Tambua kwamba kwa nafasi ambazo Mungu amekupa kuna makusudi maalum utapaswa kuyatekeleza, hivyo hakikisha unayafanya kwa uaminifu. Hata kama unafanya vizuri kwenye kusudi kuu hakikisha unakuwa makini kwenye utekelezaji wa yale mahususi.

Huwezi kuishi maisha uliyokusudiwa kama hujui kwa nini upo au unatakiwa kufanya nini chini ya jua na hivyo ni lazima ujifunze kumtafuta Mungu kwa kila hatua akusaidie kujua nini cha kufanya ili kufikia mwisho uliokusudiwa. Ndio, licha ya kusudi kuu la kuumbwa kwako  bado unahitaji kurudi kwa Mungu mara kwa mara ili kutafuta kujua nini mapenzi yake kwenye kusudi mahususi. Naam, ukiwa na aina hii ya nidhamu, utakuwa mtu  bora katika katika kutekeleza makusudi ya Mungu na ndivyo uwepo wa Mungu utakavyokuwa pamoja nawe daima (Yohana 8:28-29).   

Jambo la pili: Tafuta kujua majira (muda) uliopo yamebeba nini kwa ajili yako na kisha ushirikiane na muda kuhakikisha makusudi yanatokea (Mhubiri 3:1)

Muda umebeba mambo au makusudi yanayopaswa kufanyika. Ndani ya muda kuna makusudi au mambo yamefungwa na hivyo ni jukumu kila mtu kuyajua na kushirikiana na muda kuhakikisha yanatokea kwa yeye kufanya wajibu wake. Kusudi la uwepo wako limefungwa kwenye muda na hivyo muda wa kusudi ukiisha huna sababu ya kuendelea kuwepo duniani (Matendo ya Mitume 13:36, 17:26)

Muda wa mtu kuwepo duniani unaehasibika na haufanani na wa mtu mwingine.  Ndio, kila siku inayoongezeka inatusogeza kwenye mwisho wetu ambao haufanani kimuda. Tunahitaji neema ya kujua siku zetu za kuishi, maana ufahamu huo utatutengenezea nidhamu ya kutumia muda vizuri. Sharti tujifunze kuishi kila siku kana kwamba hiyo ndio siku yetu ya mwisho duniani (Zaburi 90:10-12)

Usijaribu kuishi kama wengine maana hujui muda wao umebeba makusudi mapana au madogo kiasi gani, bali hakikisha unakuwa mwaminifu na kutumia akili yako ipasavyo kutekeleza kusudi la Bwana wako. Kila mmoja anapaswa kufanya na kukamilisha wajibu wake kwa wakati ili kumuwezesha mwingine naye kufanya sehemu yake kwa wakati ili kufikia lengo lililokusudiwa (Mathayo 24:45-46).

Mfano: Biblia katika Luka 19:41-44 imeandikwa ‘Alipofika karibu aliuona mji, akaulilia, akisema, Laiti UNGALIJUA, hata wewe katika SIKU hii, yapasayo amani! Lakini sasa yamefichwa machoni pako. Kwa kuwa siku zitakuja, adui zako watakapokujengea boma, likuzunguke; watakuzingira na kukuhusuru pande zote; watakuangusha chini wewe na watoto wako ndani yako, wasikuachie jiwe juu ya jiwe, kwa sababu hukutambua MAJIRA ya kujiliwa kwako’Kupitia nataka uone na kujifunza mambo muhimu yafuatayo:

  • Mji ulikuwa na makosa mawili, mosi ni kutokujua mambo yapasayo amani kwa wakati uliokusudiwa na pili ni kuacha au kuruhusu adui yao awafiche wasione au wala kuja. Ndio, pale tunaposhindwa kutumia fursa zilizoachiliwa juu yetu kwa muda uliokubalika, tunafungua mlango na kumpa uhalali Shetani, kuzuia na kuficha tusione yale tuliyostahili kuyapata (Waefeso 4:18, 2 Wakorintho 11:3)
  • Kuna mambo unahitaji kuyajua na kuyafanya leo ili uweze kufanikiwa na kuwa salama kesho, naam kuufikia mwisho (destiny) uliokusudiwa. Kuna hatua unapaswa kuzichukua leo ili kuyakabili mazingira yanayokuja kesho. Mtu anapaswa daima kuishi kwa kushirikiana na nyakati zilizopo na zinazokuja mbele yake ili kuhakikisha kile kilichofichwa kwenye nyakati hizo kinaachiliwa au kinafanyika vinginevyo ni kwa hasara yake (Zaburi 90:10-12).
  • Mtu anapaswa kujua kila nyakati zilizo mbele yake zimebeba nini, zinataka nini ili ajipange kushirikiana na majra hayo kuhakikisha kile kilichobebwa kwenye nyakati hizo kinazaliwa kwa ajili ya ufalme wa nuru. Kumbuka kwamba, MUDA usiotumiwa ni sawa na mbegu uliyopewa kuipanda lakini wewe ukaitupa, naam muda usiotumiwa hauwezi kuzaa matunda yaliyokusudiwa, naam kuachilia kile ambacho muda huo ulikuwa umekibeba. (Waefeso 5:15-17).

Hitimisho: Ndugu zangu tumelala vya kutosha, tumejisahau vya kutosha, tumeshirikiana na dunia vya kutosha, ni saa ya kuamka sasa na kuyatenda kwa nguvu mapenzi ya Mungu, naam kutumika, kuomba, kuimba nk kwa nguvu mpya. Huu ni muda wa kuacha kuifuatisha namna ya dunia hii na tamaa zake bali tudumu kuzitenda  kazi za ufalme wa nuru (Warumi 13:11-12).

Utukufu na Heshima vina wewe Yesu, wastahili BWANA wangu

Pesquisar
Categorias
Leia mais
Injili Ya Yesu Kristo
AINA TATU ZA WAKRISTO
Nakusalimu katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo. Karibu tujifunze maneno matukufu ya uzima,...
Por PROSPER HABONA 2022-01-23 04:38:19 0 8KB
REVELATION
UFUNUO 18
Tukirejea kwenye ile sura ya 17 tunamwona yule mwanamke KAHABA aliyeketi juu ya yule...
Por GOSPEL PREACHER 2021-10-30 12:17:39 0 6KB
Injili Ya Yesu Kristo
MUNGU AKIKUTUMA KAZI UJUE ATAKUPA NA MAELEKEZO SAHIHI.
Ukweli ni kwamba Mungu anafanyakazi pamoja nasi hata sasa ( 2 Wakorintho 5:21). Amekuchagua ili...
Por GOSPEL PREACHER 2022-03-30 04:52:19 0 5KB
FORM 1
BASIC MATHEMATICS: FORM 1
List of all topics in Basic Mathematics for form 1 class: CLICK HERE TO VIEW. NUMBERS FRACTIONS...
Por PROSHABO ONLINE SCHOOLS 2021-10-09 12:44:29 0 5KB
HOLY BIBLE
The Healings of Jesus Christ
Individuals Who Demonstrated Faith References of Individuals Who Received Their Healing by Faith...
Por MAX SHIMBA MINISTRIES 2021-12-22 20:21:20 0 5KB